Matukio ya Picha Mchezo wa Fainali Kombe la Mapinduzi Cup 2023.Kati ya Mlandege na Singida Big Stars.Timu ya Mlandege Imeibuka Kidedea kwa Ushindi wa Bao 2-1
Benki ya CRDB Kusimamia Mfuko wa Faida Fund Unaoendeshwa na Watumishi Housing

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama amezitaka Taasisi zinazohusika na Maendeleo ya vijana, wanawake na makundi maalum kuanza kuyahamasisha makundi hayo kuwekeza kwenye Mfuko wa Faida uliopo chini ya Shirika la Watumishi (Watukishi Housing Investiments), ili asiwepo mtanzania wakuachwa nyuma katika shughuli za uwekezaji na ukuzaji wa mitaji.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mfuko huo uliofanyika kwenye ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es salaam, Waziri Jenista amesema mfuko huo ni salama kwa uwekezaji kwani tangu uanzishwe hadi sasa umeonesha mafanikio makubwa kwenye sekta ya uwekezaji na uchumi.

Aidha amebainisha kuwa umiliki wa mfuko huo haubagui kufuatia kiwango cha chini cha uwekezaji kuwa ni kuanzia elf 10 hivyo unatoa fursa Kwa mtanzania yoyote kujiunga.
Kwa upande wa Mtunza Amana wa Mfuko wa Faida (Faida Fund) ambaye ni Benki ya CRDB kupitia kwa Mkurugenzi Mtendaji wake, Abdulmajid Nsekela ameeleza kwamba mfuko huo ni wa kipekee, kwani umezingatia sera mahususi ya huduma jumuishi za kifedha zinazomjali mtanzania wa rika zote ikiwa ni pamoja na kuweza kununua vipande kwa shilingi elfu 10 jambo ambalo linaenda sambaba na sera ya benki hiyo ya kumsikiliza mteja.

Amebainisha kuwa Benki ya CRDB inachangia Zaidi ya asilimia 70 ya wateja wote wanaoshiriki katika masoko ya mitaji na dhamana ambapo Soko la Hisa la Dar es Salaam-DSE kupitia tuzo zake inaitabmbua benki hiyo kama kinara wa huduma bora kwenye masoko ya mitaji.
Aidha amefafanua kwamba, Mfuko wa Faida unakuwa mfuko wa saba katika mifuko ya uwezazaji wa pamoja ambayo benki ya crdb inaisimamia na unatoa fursa pekee ya uwekezaji wa muda mfupi kwa watanzania kuweza kukuza mitaji yao kwa faida lakini pia ni faida kwa watumishi housing kukusanya fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Hata hivyo amesema kuwa benki imejipanga kusimamia mfuko kikamilifu na kuhakikisha maslahi ya wawekezaji yanalindwa kulingana na waraka wa makubaliano kati ya watumishi housing na crdb katika usimamizi wa mfuko huo.


Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mfuko wa Faida (Faida Fund), uliofanyika kwenye ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es salaam, Januari 14, 2023.






ZAIDI YA VIJANA 300 WA UVCCM IRINGA WAMEJITOKEZA KUCHANGIA DAMU IRINGA
Jamii yatakiwa kukutana kujadili kero zinazowakabili
“Haki haisubiriwi, haki inatafutwa, ni lazima wananchi wawe na uelewa wa kutosha juu ya zipi ni haki zao”- WADAU
ZANZIBAR
KATIKA kuhakikisha jamii inakuwa na uwezo wa kutambua umuhimu wa kudai upatikanaji wa haki zao za msingi, kamati za wananchi kutoka shehia za Wilaya za Micheweni, Wete, Mkoani na Chake Chake Pemba zimeshauriwa kuendelea kuwashirikisha wananchi kujadili changamoto zinazowakabili ili kuzipatia ufumbuzi kwa njia na wakati sahihi bila kusababisha madhara.
Ushauri huo umetolewa wakati wa mkutano na kamati za wananchi kutoka shehia za wilaya hizo kisiwani Pemba ulioandaliwa na Jumuiya ya Utetezi wa Mazingira na Jinsia Pemba (PEGAO) kwa kushirikiana na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ) kwa lengo la kuzijengea uwezo kamati hizo kufuatilia kero zinazokwaza haki za wanawake ambazo ziliibuliwa na wahamasishaji jamii kwenye maeneo yao.
Akizungumza katika mkutano huo ambao ni utekelezaji mradi wa kuwawezesha wanawake kwenye uongozi unaofadhiliwa na Ubalozi wa Norway Tanzania, afisa tathimini na ufuatiliaji wa TAMWA ZNZ, Moh’d Khatib, alihimiza jamii kuwa na utamaduni wa kukutana kujadili kero zinazowakabili na kukwaza haki za wanawake ili kuzitaftia suluhu kwa pamoja.
Alisema, “lazima kamati hizi zikutane na wananchi ili wao wenyewe waseme wana changamoto gani kuliko kuwasemea, hii itasaidia kuwa na uthibitisho na ushahidi wa kutosha juu ya changamoto yoyote inayotafutiwa ufumbuzi.”
Alibainisha kupitia ushirikishwaji wa wananchi kujadili changamoto na kero zinazowakabili wanawake kupata haki zao itasaidia kukuza uelewa wa jamii kushiriki moja kwa moja kudai haki zao.
“Kupitia kamati za shehia, wananchi wote wanatakiwa wawe na uwezo wa kutambua changamoto zao na wajue kuwa ni wajibu wao kuzitaftia ufumbuzi na kudai haki zao kwa kujua nani anapaswa kuzitatua ili wachukue hatua wenyewe katika kuhakikisha wanapata haki muhimu hasa wanawake,” alifahamisha.
Aidha aliongeza kuwa Ubalozi wa Norway kwa kushirikiana na TAMWA, ZAFELA na PEGAO kupitia mradi huo unalenga kujenga jamii imara yenye uwezo wa kupaza sauti kwenye kero zinazopelekea kuwakosesha wanawake haki za msingi katika jamii.
“Lengo kubwa la mradi huu tunataka kujenga jamii ya wananchi wenye uthubutu wa kupaza sauti juu ya changamoto zinazowakabili kwenye maeneo yao hasa wanawake ili kusaidia utatuzi wa kero hizo kwa wakati,” alisema afisa huyo.
Mapemba mkurugenzi wa mradi huo kwa upande wa PEGAO, Hafid Abdi, alifahamisha jamii inapaswa kutambua kwamba inao wajibu wa kukabiliana na changamoto zinazowakabili ili kujenga jamii yenye kufuata misingi ya usawa wa kijinsia kwa wote katika kila eneo.
Alieleza, “wananchi wanatakiwa wajue kwamba kero zilizopo katika jamii ni zao na wanao wajibu wa kuzitaftia ufumbuzi kwa njia sahihi ili kuwepo na misingi ya upatikanaji wa haki za msingi kwa kila mmoja hasa wanawake katika nyanja zote ikiwemo kiuongozi.”
Nae Mratibu TAMWA ZNZ ofisi ya Pemba, Fat-hiya Mussa, alisema “haki haisubiriwi, haki inatafutwa, hivyo ni lazima wananchi wawe na uelewa wa kutosha juu ya zipi ni haki zao na namna gani wanapaswa kudai haki zao kwa njia iliyo sahihi.”
Mapema Mohamed Abdalla mjumbe wa kamati hizo alihimiza jamii kutumia vyombo vya habari kupaza sauti zao ili changamoto zinazowakabili ziweze kuwafikia walengwa kwa wakati.
Alibainisha, “ili changamoto hizi ziweze kutatuliwa, ni lazima sisi wananchi katika kila maeneo ambayo tunaona ni kikwazo kwetu tupate wandishi wa habari ambao watatusaidia kupasa sauti zetu.”
Rais Mhe Samia awapongeza vijana wa Kitanzania kwa kupata medali ya Fedha
*Ni baada ya kuibuka washindi wa pili katika mashindano ya ubunifu duniani
MHESHIMIWA Rais Dkt. Samia Suluhu Hssan amewapongeza vijana wa Kitanzania walioibuka washindi wa pili na kupata medali ya fedha katika mashindano ya kwanza ya Global Robotics Challenge yaliyofanyika Geneva Uswisi na kushirikisha mataifa zaidi ya 190.
Amefarijika kusikia kuwa roboti iliyoundwa na vijana kutoka Tanzania chini ya maudhui ya kukamata hewa ukaa (Carbon dioxide) inaweza kusaidia kusafisha kaboni hewani na kusaidia kupunguza ongezeko la joto kwenye angahewa ya Dunia.
Kauli hiyo imetolewa leo (Jumapili, Januari 15, 2023) na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia katika hafla ya kuwapongeza vijana hao iliyofanyika kwenye ukumbi wa Ofisi Ndogo ya Waziri Mkuu, Magogoni jijini Dar es Salaam.
Amesema hayo ni mafanikio makubwa na Watanzania wote wanapaswa kujivunia kwa kuiwakilisha nchi yetu vizuri. “Nitumie nafasi hii kuwaahidi kuwa Serikali kupitia Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari itaendelea kufuatilia maendeleo yenu na kuona namna ya kuendeleza vipaji vyenu. ”
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kuielekeza Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari iandae mpango wa kuwa na vituo vya ubunifu nchini katika ngazi za Mikoa na Wilaya mbalimbali ili kusaidia kuinua vipaji vya vijana.
Amesema Wizara iimarishe utaratibu wa kuwatambua na kuwaendeleza wabunifu mbalimbali ili kuwamotisha na kukuza ajira nchini na ishirikiane na mamlaka husika kuandaa utaratibu wa kuwasaidia wabunifu mbalimbali na kuwaunganisha na taasisi pamoja na makampuni kwa ajili ya kuendeleza bunifu za kazi zao kulingana na mahitaji.
Vilevile Waziri Mkuu ameielekeza Wizara hiyo na mamlaka husika zijipange kuwekeza katika kulinda usalama wa taarifa za watumiaji wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA sambamba na kutoa elimu kuhusu usalama sahihi wa vifaa na matumizi salama ya mifumo ya kompyuta.
Amesema Wizara hiyo kupitia Tume ya TEHAMA ifanyie kazi vikwazo mbalimbali vya kisera na kikodi vinavyoleta changamoto kwa wabunifu katika masuala ya TEHAMA na matokeo ya bunifu mbalimbali yawekewe utaratibu wa kubidhaishwa/kupata soko badala ya kuwekwa maktaba.
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ameipongeza Kampuni ya Mawasiliano ya Tigo kwa kuamua kutumia sehemu ya mapato yao kwa kuwasaidia vijana wa kike nchini katika kuendeleza bunifu nchini kupitia APPS and Girls.
Waziri huyo mesema kuwa takwimu mbalimbali zinaonesha kuwa ushiriki wa mabinti na wanawake katika matumizi ya TEHAMA si mzuri sana, Barani Afrika asilimia 24 tu ya wanawake wanashiriki kwenye TEHAMA huku wanaume ni asilimia 35.
”Tanzania ukienda mashuleni watu wanaosoma Computer Science na mambo yanayohusiana na TEHAMA wanawake ni asilimia 10 tu, ni muhimu kuendelea kuongeza nguvu katika kupunguza pengo hilo. ”
Naye, Afisa Mkuu wa Udhibiti Kampuni ya MIC Tanzania PLC (TIGO), Innocent Rwetabula amesema kampuni yao inafanya kazi kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali kwa sekta ya mawasiliano na kuongoza safari ya kidigitali hadi kufikia Tanzania ya kidigitali.
Amesema uwezeshaji wa wasichana ni mojawapo ya programu zao kuu za uwajibikaji kwa jamii kwa lengo la kuwawezesha wasichana walio katika shule za sekondari na wale walioacha shule kwa sababu mbalimbali wenye umri wa kuanzia miaka 12 hadi 24 kupata ujuzi wa kidigitali na stadi za ujasiriamali.
Amesema lengo la ufadhili huo ni kuziba pengo kati ya wavulana na wasichana katika sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM), kutoa ujuzi na stadi za ujasiriamali kupitia utoaji wa mafunzo ya TEHAMA, ushauri na uanzishaji wa biashara mpya za kiteknolojia ambapo mwaka jana wasichana 1,590 walinufaika na mpango huo.
Akizungumzia kuhusu shindano la kwanza ya Global Robotics Challenge amesema hufanyika kila mwaka kwa mtindo wa Olimpiki na kauli mbiu ya mwaka huu ilikuwa ni cabon capture, ambayo ni mchakato wa kukamata hewa ukaa iliyopo na kuzuia isiingie angani. Kundi la wanafunzi watano kati ya 11 waliiwakilisha nchi na kupata nafasi ya pili.
Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi wenzake, Maria Mtega ambaye anasoma kitado cha pili shule ya sekondari ya St.Theresa amesema anashukuru kwa mafunzo waliyoyapa ambayo yamewezesha kupata nafasi ya pili na pia wataendeleza vipaji vyao na hatimaye waweze kuwa wabunifu wakubwa nchini.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, JANUARI 15, 2023.
Taarifa kwa Vyombo vya Habari
Rais Dk Hussein Mwinyi akutana ujumbe wa Viongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa Ikulu

Mwenyekiti wa UWT Taifa Ndg Mary Chatanda akikabidhi Tuzo ya Pongezi kwa Mhe Dkt Hussein Ali Mwinyi kwa kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti CCM Zanzibar na Kutekeleza Ilani ya CCM ya Uchaguzi 2020-2025. #UWTImara #JeshiLaMama #KaziIendelee

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar Dkt Hussein Ali Mwinyi akiteta jambo na ujumbe wa Viongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa Ikulu Zanzibar mapema leo

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar Dkt Hussein Ali Mwinyi akiteta jambo na ujumbe waViongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa Ikulu Zanzibar mapema leo


Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar Dkt Hussein Ali Mwinyi akiwa kwenye picha ya pamoja na Makamu Mwenyekiti wa UWT Taifa Ndugu Zainab Shomari mara baada ya kuteta na Viongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa Ikulu Zanzibar mapema leoujumbe ambao uliongozwa na Mwenyekiti wa UWT Taifa Ndugu Mary Chatanda. |
![]() |
Ndg Riziki Kingwande, Naibu Katibu Mkuu UWT - Bara |

Na Mwandishi WetuZanzibar.
Makamu Mwenyekiti CCM Zanzibar,Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi leo Jumatatu Januari 16,2023 amekutana na Viongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Ikulu Zanzibar.
Uongozi wa Jumuiya hiyo uliongozwa na Mwenyekiti wa UWT Taifa Ndugu Mary Chatanda ,Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa aliyeambatana na Makamu Mwenyekiti UWT Zanzibar Ndugu Zainab Shomari ,viongozi mbalimbali wa kitaifa wa Jumuiya hiyo kwa nia ya kujitambulisha baada ya kuchaguliwa .
Pia wamempongeza Dk.Hussein Ali Mwinyi kwa kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti CCM Zanzibar na Kutekeleza Ilani ya CCM ya Utekelezaji 2020-2025 .
Kamati ya Bunge ya Sheria Ndogo Yapokea Taarifa ya Wizara ya Utamaduni
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo imepokea taarifa ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kuhusu hoja mbalimbali za uchambuzi kuhusu Kanuni ziitwazo Licensing and Rights To Benefit From Re- Sale, Regulations ambazo zimeanzishwa na Sheria ya HakiMiliki na Hakishiriki.
Akiwasilisha Taarifa hiyo, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe.Pauline Gekul amesema, wizara imefanyia kazi hoja mbalimbali ilizoagiza na Bunge katika vikao vya Kamati vya mwezi Aprili 2022.
"Wizara imepokea Hoja 06, kutoka katika Kamati na imezifanyia kazi kupitia Ofisi ya Hakimili na Hakishiriki ( COSOTA) ikiwemo kuzifuta baadhi ya Kanuni na kutengeneza nyingine ambazo zipo Ofisi ya mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kuhakikiwa na kupewa kibali" amesema Mhe.Gekul.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe.Gaston Rwekiza ambaye ni Mbunge wa Bukoba Vijini ameelekeza wizara kukamilisha mchakato wa kutengeneza Kanuni hizo, mapema na kuziwalisha kwa Kamati hiyo kwa ajili ya hatua zinazofuata.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu Said Yakubu, Afisa Mtendaji Mkuu wa COSOTA Bi. Doreen Sinare na Viongozi wengine wa Wizara.
MAJALIWA: Tulinde Mbolea ya Ruzuku Iliyotolewa na Rais Dkt.Samia Suluhu
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wananchi kuwa walinzi wa mbolea ya ruzuku iliyotolewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kuhakikisha inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa ya kuongeza uzalishaji wa mazao katika msimu wa 2022/2023 litimie.
Amesema kuwa kumekuwa na watanzania wachache wasiokuwa na nia njema wanaotorosha mbolea kwenda nchi jirani na kuwaacha watanzania bila kuwa na mbolea ya kutosha ”jambo hili lazima tulikemee na tulisimamie sote ili kuhakikisha mbolea iliyopo nchini ni kwa ajili ya watanzania, kila mmoja awe mlinzi kwa mwenzake”
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumatatu, Januari 16, 2023) wakati akisalimia na wananchi kwenye eneo la Mbalizi jijini Mbeya akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali. Amesema utoaji wa ruzuku hiyo ya mbolea unalenga kuongeza uzalishaji wa chakula nchini na ni marufuku kuiuza nje.
Ameongeza kuwa awali mbolea iliuzwa kwa zaidi ya shilingi 100,000 lakini Mheshimiwa Rais Dkt. Samia akaridhia kutoa ruzuku shilingi bilioni 150 ili ikashushe bei ya mbolea na sasa inauzwa kwa shilingi 70,000. ”Tusikubali fedha hiyo kutumika nje la malengo, tulinde mbolea yetu isiuzwe kwa wasiohusika.”
”Nimefurahi sana kwa hatua zilizochukuliwa mkoani Songwe, tani 2199 zimekamatwa zikipelekwa nchi jirani hii haikubaliki, watanzania tuwe walinzi hii ni pesa yetu inatoroshwa na wachache, malengo yetu ni kuwahudumia ninyi kwa usimamizi wa Rais Dkt. Samia”
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kuelekeza hatua zilizofikiwa katika maendeleo ya uboreshwaji wa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Songwe kuwa tayari njia ya kurukia ndege imekamilika kwa asilimia 100, jengo la abiria ujenzi umefikia asilimia 96 na sasa zoezi la ufungaji taa linaendelea na litakapokamilika uwanja huo utatumika wakati wote.
”Tunafanya hivi ili kuvuta masoko kutoka nchi jirani ikiwemo Kongo, Zambia na malawi walete ndege zako, haya yote yanafanywa na Rais wetu Dkt. Samia kwasababu ana maono ya mbali na dhamira yake ya dhati ya kuwaletea watanzania maendeleo.”
Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ameidhinisha kiasi cha shilingi bilioni 3.3 kwa ajili ujenzi wa mradi wa maji wa Shongo - Igale ambao umekamilika na watu wanapata huduma ya maji.
Ameongeza kuwa, pamoja na mahitaji ya maji katika eneo la mbalizi kuwa lita milioni 8, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia alitoa shilingi bilioni. 4.8 kwa ajili ya kujenga mradi wa maji wa Inunga ili kuongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 8 hadi 12.
Naye, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, David Silinde amesema Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 580 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 29 katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ambapo yote yamekamilika kwa asilimia 100 na yanatumika.
Awali, baadhi ya wananchi walimuomba Mheshimiwa Majaliwa awasaidie katika kutatua changamoto ya fidia iliyotokana na kupisha ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe tangu mwaka 2002, ambapo Meneja wa uwanja huo, Mhandisi Danstan Komba alisema wanachodai wananchi hao ni mapunjo ya fidia.
Alisema baada ya eneo lao kutwaliwa walilipwa fidia ambapo baadae yalitokea malalamiko ya mapunjo ya fidia ambapo timu ya uchunguzi ya suala hilo iliundwa na ilishafika katika eneo hilo, hivyo aliwaomba wananchi watulie wakati suala lao linaendelea kufanyiwa kazi.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATATU, JANUARI 16, 2023.
Taasisi zinazoendelea na ujenzi wa Ofisi zatakiwa kukamilisha majengo yao kwa wakati Jijini Dodoma
Serikali imeziagiza Taasisi zote zinazoendelea na ujenzi wa majengo ya Ofisi zao Jijini Dodoma kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa kuzingatia taratibu zote za ujenzi ikiwemo ubora, muda, bajeti iliyotengwa na thamani ya fedha ili kuleta tija inayotarajiwa.
Maagizo hayo yametolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. George simbachawene wakati wa hafla ya kukabidhi Vibali vya Ujenzi wa Ofisi za Taasisi za Serikali Dodoma iliyofanyika katika Ukumbi wa Hazina mapema.
Waziri Simbachawene amesema, kila Taasisi ya Serikali ihakikishe inajenga majengo ya Ofisi zake ili kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhamishia Makao makuu yake Dodoma na kuifanya Dodoma kuwa eneo lenye ufanisi.
“Taasisi zote zilizoelekezwa kuhamia Dodoma kwa mujibu wa ratiba niliyoitoa leo zihakikishe zinatekeleza maagizo hayo na Makatibu Wakuu wa Wizara husika wahakikishe wanasimamia mpango kazi wa utekelezaji wake,”alisema Mhe.Simbachawene
Aliongezea kuwa, Mpango huu ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 151 chini ya kifungu (a), (b) na (c) vinavyoielekeza Serikali kutunga Sheria ya kuitambua Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi na kuhakikisha kwamba majengo ya Wizara na Taasisi yanajengwa Dodoma badala ya Dar es Salaam.
Aidha Waziri ameagiza Ofisi ya Katibu Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu kwa kushirikiana na Mamlaka husika kuendelea kuratibu Mpango wa Serikali na taasisi zake kuhamia Dodoma pamoja na ujenzi wa miundombinu ya kiuchumi na uboreshaji wa huduma mbalimbali za kijamii Dodoma.
Sambamba na hilo, Serikali imekamilisha ratiba na mwongozo utakaowezesha Taasisi za Serikali ambazo bado zinaendelea kutekeleza majukumu yake Dar es Salaam kuweza kuhamishia shughuli zao Jijini Dodoma kwa awamu.
“Katika utekelezaji wa suala hili, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwamba Taasisi 42 zihamie Dodoma ndani ya mwaka huu wa fedha wa 2022/23; Taasisi 36 zitahamia Dodoma katika mwaka ujao wa fedha wa 2023/24 na Taasisi 19 zitahamia katika mwaka 2024/25 wakati Taasisi 27 zimeelekezwa, kwa kuzingatia aina ya majukumu zilizonazo, kuendelea kutekeleza majukumu yake Mkoani Dar es Salaam.” Alieleza.
Alisisitiza kuwa, hatua hii itakamilisha sehemu kubwa ya Mpango wa Serikali wa kuhamia Dodoma ambapo hadi sasa tayari Taasisi 65 zilishahamia Dodoma tangu mwaka 2016 hadi 2022.
Waziri ameziagiza Taasisi nyingine ambazo bado hazijaanza maandalizi ya ujenzi wa Ofisi za serikali Dodoma ziwasilishe Ofisi ya Waziri Mkuu Mahitaji ya Viwanja vya ujenzi wa Ofisi za taasisi Dodoma kwa ajili ya uratibu wa pamoja.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu ya kuwezesha taasisi kuwepo.
“Tunaishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi kubwa mnayoifanya kwa kupanga makao makuu ya serikali yetu yanakuwa ni mji wa kisasa na mji uliopangwa.”alisema Mhe. Rosemary.
Awali Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Dkt, John Jingu akitoa taarifa ya utekelezajia amesema Ofisi ya waziri Mkuu imeidhinisha vibali 55 kwa nyakati tofauti kuanzia mwaka 2018 kati ya hizo taasisi 20 zimekamilisha ujenzi, taasisi 16 zinaendelea na ujenzi na taasisi 19 zimeanza maandalizi ya ujenzi.
“Majengo haya yanajengwa katika maeneo mbalimbali, na ujenzi huu unazingatia mpango kabambe wa Jiji la Dodoma.”
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Akutana na Kufanya Mazungumzo na Balozi wa Cuba Na Indonesia Ofisi Ndogo ya CCM Lumumba Dar Es Salaam
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana akizungumza na Balozi wa Cuba, Yordenis Despaigne Vera, alipofika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, leo Januari 16, 2023.
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana akifurahi na kushikana mikono na Balozi wa Cuba, Yordenis Despaigne Vera, mara baada ya kumaliza mazungumzo yao alipofika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, leo Januari 16, 2023.
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana akiagana na Balozi wa Cuba, Yordenis Despaigne Vera, alipofika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, leo Januari 16, 2023.
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana akisalimiana na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mheshimiwa Triyogo Jatmiko alipofika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, leo Januari 16, 2023.
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana akimsikiliza Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mheshimiwa Triyogo Jatmiko wakati wa Mazungumzo yao alipofika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, leo Januari 16, 2023.
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana akiagana na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mheshimiwa Triyogo Jatmiko alipofika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, leo Januari 16, 2023.
Waziri Mkuu - Akutana na vijana wa Kitanzania waliobuni roboti ya kukamata hewa ukaa (Carbon dioxide)
Ndg. Sophia Mjema Awasili Ofisini Kwake Ofisi Ndogo ya CCM Lumumba. Kazi Imeanza Hakuna Kusubiri
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa (NEC) Idara ya Itikadi na Uenezi Ndugu Sophia Edward Mjema amewasili Ofisini kwake Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba Dar es Salaam leo Jumatatu tarehe 16 Januari, 2022.
Ndugu Mjema akizungumza na watumishi na maafisa wa idara yake amewataka kutekeleza majukumu yao kwa bidii, umoja, ubunifu na wakati wote kuhakikisha wanakuwa mfano bora katika kuendelea kujenga, kutunza na kulinda haiba nzuri ya CCM na Mwenyekiti wake Rais Dkt Samia Suluhu Hassan.
Amesisitiza kazi kubwa iliyopo mbele ni kuendelea kuyasema mazuri yanayofanyika kwa wananchi ili wayafahamu, kueleza uzuri wa CCM, kuwasikiliza wananchi kero au changamoto zao ili kuzitafutia ufumbuzi, kufuatilia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi na kuendelea kuwajengea uwezo wanachama na viongozi wetu kupitia mafunzo. Kazi zote hizi hazipaswi kusubiri, tuanze sasa na tuendelee mbele. @ccmtanzania @sophia_mjema
#CCMImara #RaisNiSamia #KaziIendelee.
Naibu Katibu Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar Ndg.Shomari Apongeza Jitihada za Viongozi Wakuu Katika Kuimarisha Mawasiliano Nchini
Naibu katibu Wizara ya Ujenzi,Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar Ndugu Shomari Omar Shomari amepongeza jitihada zinazochukuliwa na viongozi wa kuu wa Nchi katika uimarishaji wa huduma za Mawasiliano ya Teknolojia ya Habari.
Naibu katibu Mkuu Shomari ameeleza hayo wakati akikifungua kikao kazi kilichowashirikisha wadau mbalimbali kutoka katika Wizara na Taasisi za Serikali kilichotoa maoni yatakayowezesha kupata taarifa za ufanikishaji wa upembuzi yakinifu wa mradi wa ujenzi wa maghala ya kuhifadhi bidhaa za biashara mtandao.
Amesema kikao hicho ni matokeo ya ziara za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi Nchini Oman ambapo wameoneshwa kuvutiwa kwao na huduma zinazotolewa na Shirika la Posta la Oman (ASYAD) kutokana na mifano wanayotumia katika kufanya biashara mtandao.
Naibu katibu Shomari amefafanua kwamba utekelezaji huo wa uimarishaji wa huduma za teknolojia ya Habari na Mawasiliano unakwenda sambamba na mpango wa dira ya Maendeleo ya Serikali 2050 pamoja na ilani ya uchaguzi ya CCM 2020 – 2025.
Wakizungumza mara baada ya kikao hicho Mkurugenzi wa idara ya Mawasiliano na Mkurugenzi wa Jackson Group Kelvin Twissa wamesema mpango huo utakapo kamilika utaiwezesha Nchi kufungua fursa zaidi kwa wananchi wake kwa kufanya biashara kwa kutumia njia ya mtandao sambamba na kurahisisha upatikanaji wa bidhaa mbalimbali.
Wakurugenzi hao wameeleza kuwa Tanzania ipo katika nafasi nzuri kwa kutumia miundombinu yake katika kusambaza bidhaa zake kwa nchi zilizo katika ukanda wan chi za Sahara.
Aidha wamefafanua kwamba ujenzi wa maghala ya kuhifadhia bidhaa hapa Nchini utaongeza wigo kwa Taasisi za ukusanyaji wa Mapato kukusanya zaidi kutokana na kampuni nyingi kupitisha bidhaa zake Tanzania.
Wadau kutoka taasisi mbalimbali wameshiriki katika kikao hicho kwa ajili ya kutoa taarifa zitakazo wezesha kufanikisha kazi hiyo ya upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa maghala ya kuhifadhia bidhaa za biashara mtandao Tanzania.
Taasisi hizo zina jumuisha Shirika la Bandari Zanzibar, ZICTIA, ZMA, KILIMO, BIASHARA, ZRA, Pamoja na wadau wengine.
Imetolewa na kitengo cha Habari (WUMU)
Januari 16, 2023.
Ahukumia Miaka 30 kwa Kosa la Kulawati
Na Masanja Mabula PEMBA
Serikali Yamaliza Mgogoro wa Ardhi Bonde la Usangu - Mhe.Majaliwa *Yaridhia kutoa eneo la hekta 74,000 kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wadau waliowekeza katika Bonde la Usangu, ikiwemo wakulima wa mpunga na wafugaji, kwenye ukumbi wa Eden jijini Mbeya Januari 16, 2023. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
SERIKALI ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeumaliza mgogoro wa matumizi ya ardhi wilaya Mbarali mkoani Mbeya uliodumu kwa miaka 15 ambao ulihusisha wakazi wa wilaya hiyo katika eneo la Bonde la Usangu dhidi ya hifadhi ya Taifa ya Ruaha.
Akizungumza katika kikao na wadau waliowekeza katika Bonde la Usangu wakiwemo wakulima wa mashamba ya mpunga, mashine za kukoboa mpunga na wafugaji katika vitalu kilichofanyika jana (Januari 16, 2023) mkoani Mbeya, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imefanya maboresho makubwa kwenye Tangazo la Serikali namba 28 ambayo itawawezesha wananchi kufanya shughuli za kilimo na ufugaji endelevu.
Amesema marekebisho ya tangazo hilo yatawezesha baadhi ya vitongoji vilivyokuwa vimetangazwa awali kuwa ndani ya hifadhi kuachwa nje ya mipaka ikiwemo kutoa eneo la hekta 74,000 kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji.
“Hii GN 28 Serikali tumeamua kuitafutia ufumbuzi baada ya vikao vingi na wadau kwa faraja kabisa nataka niwaambie tumefikia hatua nzuri itakayowezesha kila anayejishughulisha na kilimo kuendelea na kilimo chake na kila anayejishughulisha na mifugo kuendelea na ufugaji yake.”
Amesema kuwa Serikali inataka kuhakikisha Wilaya ya Mbarali inaendesha shughuli za kilimo kitaalam na kwa tija. “Tumeona maendeleo makubwa na ujenzi wa viwanda vya mtu mmoja mmoja na vikundi, Serikali inataka kuona shughuli hizo zinakuwa endelevu, tunataka mpanue viwanda vyenu na mzalishe zaidi.”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali imeamua kuitoa nje ya hifadhi ranchi ya Usangu kwa ajili ya shughuli za ufugaji wa kisasa. “GN namba 28 iliingiza ranchi ndani ya hifadhi, lakini ili wafugaji wawe huru tumeindoa na hivyo itakuwa nje, tumeacha na mito kadhaa ambayo itahifadhiwa kwa sheria za mazingira.”
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amewataka wafugaji kujiamini kwani mifugo ni uchumi. “Tunataka tuondokane na uchungaji na kuwafanya Watanzania wafugaji kuacha kutembea umbali mrefu na ng'ombe kwani inaondoa thamani ya nyama, tunataka mfuge kisasa.”
Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angelina Mabula amesema kuwa maeneo ambayo yameondolewa katika hifadhi watahakikisha mpango bora wa matumizi ya ardhi unawekwa ili wananchi waweze kufanya kile ambacho kimepangwa kufanyika kwa wakati huo.
Ameongeza kuwa watahakikisha wananchi hao wanapata hati miliki za maeneo yao ili waweze kuzitumia katika shughuli mbalimbali za maendeleo na mpango wa uandaaji utafanyika kwenye vijiji vyote vinavyohusika.
Naye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Dkt. Selemani Jafo amesema kuwa kwenye maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji watumiaji wote wanapaswa kuheshimu sheria ya mazingira.
Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi Dkt. Pindi Chana amewataka watumiaji wa eneo lililotolewa kwa ajili ya shughuli za ufugaji na kilimo waendelee kulilinda eneo lililobaki. “Tusifuge wala kulima katika eneo lililobaki eneo hili ni chanzo kikubwa cha maji na sehemu ya utalii”.
Naye, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amesema ranchi ya Usangu ni kwa ajili ya shughuli za ufugaji tu na isitokee yeyote akafanya tofauti na lengo. “Tulioko kwenye ranchi tufuge, wengine mnabadilisha matumizi wengine hamfugi lakini mnakodisha watu wanakuja kulima kwenye vitalu, wale mnaolima badala ya kufuga tutawanyang’anya vitalu.”
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, JANUARI 17, 2023.
Mabodia Zaidi ya 20 Kupanda Ulingoni Januari 18 na 28 Jijini Tanga Kuoneshana Umwamba,Ibrahim Classic,Matumla Wamo
MASHABIKI wa ngumi mkoa wa Tanga wanatarajiwa kushuhudia pambano la ngumi la kufungua mwaka 2023 wakati w mabondia Mustafa Doto kutoka Dar es Salaam atakapopambana na Said Mundi kutoka Tanga katika mnyukano wa round 10 kesho Januari 18, 2023.
Akizungumza na waandishi wa Habari Jijini hapa leo, Promota maarufu nchini, Ali Mwazoa na ambaye pia mtayarishaji wa pambano hilo alieleza kutakuwa na mengine ya utangulizi 9.
Mapambano hayo yatakuwa kati ya Jay Jay atakayepambana na Peter Julius wakati Jonas Mtafya atapigana na Patrick Kimweri. Wengne ni Hamis Mwambashi dhdi ya Haji Juma, wote kutoka Tanga.
Mtoto wa bondia mkongwe nchini, Rashid Matumla, Snake Junior atapambana na Ali Reli wote kutoka Tanga..
Haya ni mapambano ya utangulizi kwa ajili ya mabondia chipukizi kuelekea pambano kubwa la aina yake mkoani na nchini Tanzania kati ya mabondia wawili wanaogopwa, Ibrahim Classic atakayemkabili bondia mwenye mikwara na ngumi nzito, Ndondande Harmer, wa nchini Zimbabwe. Pambano hilo litakuwa la round 10.
Promota Mwazoa alitoa wito kwa mashabiki wa jijini Tanga na nje ya mkoa kujitokeza kwa wingi kushuhudia mabambano hayo mawili yatakayofanyika 18 na 28 Januari ambayo yatautangaza mkoa katika fursa za biashara na ajira.
Pia Mwazoa aliahidi kuandaa mapambano mengine ya ngumi ambayo yatatoa zaidi fursa kwa vijana wanaochipukia katika ulingo wa michezo ya ngumi nchini.
Timu ya Mlandege Mabingwa na Kombe la Mapinduzi Cup 2023 Wakishangilia Ubingwa Wao Uwanja wa Amaan Zanzibar
Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan ahudhuria Ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum), Davos, nchini Uswisi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa pamoja na viongozi mbalimbali kwenye ufunguzi wa Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum) uliofanyika katika Ukumbi wa Congress, Davos nchini Uswisi tarehe 17 Januari, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na kuzungumza na Washiriki pamoja na viongozi mbalimbali wanaohudhuria Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum) uliofanyika katika Ukumbi wa Congress, Davos nchini Uswisi tarehe 17 Januari, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisikiliza kwa makini kutoka kwa mmoja wa Washiriki wanaohudhuria Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum) uliofanyika katika Ukumbi wa Congress, Davos nchini Uswisi tarehe 17 Januari, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani Dkt. Abdallah Possi mara baada ya kuhudhuria ufunguzi wa Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (World Economic Forum) uliofanyika katika Ukumbi wa Congress, Davos nchini Uswisi tarehe 17 Januari, 2023.