Mstahiki Meya wa jiji la Zanzibar Mahmoud M, Mussa amewasisitiza vijana kuwa wazalendo na kuwacha kujishirikisha na vitendo viovu vikiwemo vya udhalilishaji na matumizi ya dawa za kulevya ili taifa lipate viongozi bora.
Akifungua mafunzo elekezi kwa viongozi vijana yalioyoandaliwa na Raha Tv Online Mahmoud amesema viongozi vijana wanamchango mkubwa katika kuchochea maendeleo kwa taifa lao hivyo si vyema kutumika katika vitendo viovu ambavyo vinarejesha nyuma maendeleo ya taifa na hatimae kushiriki kikamilifu katika kuinua uchumi wa nchi.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi Mkuu wa Wilaya ya Magharibi B Suzan Peter Kunambi amewataka.vijana kutokata tamaa katika kuzisimamia ndoto zao ili zikamilike sambamba na kuutaka uongozi wa Raha Tv Online kuwa wabunifu ili jamii ifaidike na habari mbali mbali ikiwemo za kuelimisha na kuburudisha .
Katibu Mtendaji Tume ya Utangazaji Zanzibar Suleiman Abdullah amesema Tume kwa kushirikiana na TCRA zitaendelea kuvisimamia vyombo vya habari nchini ili kuona vinafuata utaratibu na maadili ya utangazaji.
Mkurugenzi Mkuu wa Raha Tv Online ndugu Raya Hamad Mchere amesema Raha Tv Online inalengo la kuwapasha habari vijana na wanawake na jamii kwa ujumla kuhusu mambo mbali mbali ikiwemo kuhabarisha, kuelimisha, kuhamasisha na kuburudisha
Mafunzo hayo yaliyobeba ujumbe ‘MIMI NI WA THAMANI’ yana lengo la kuwajengea uwezo Viongozi vijana na kuwawezesha kujua thamani yao na umuhimu wao kwa nchi, kwa vile wana wajibu wa kuhakikisha kuwa wanathamini jitahada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuwainua kiuchumi na hatimae malengo yao kufanikiwa.
Mafunzo hayo yamewashirikisha viongozi vijana kutoka Baraza la Vijana Zanzibar, Vyuo Vikuu viliopo Zanzibar na wengine kutoka taasisi zisizo za kiserikali ambapo Mkurugenzi huyo amaesema mafunzo elekezi yatakuwa chachu ya kufahamu kwa kina changamoto za vijana na njia za kuwajengea uwezo ili wawe vijana wazalendo na kufuata sheria za nchi hii bila kushurutishwa.
Mafunzo hayo yamefungwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ndg Muhammed Ali Abdalla ‘teacher Muha’ ambapo ameupongeza uongozi wa Raha Tv Online kwa kuwa na malengo mazuri ya kuwajengea misingi imara kwa kuamsha ari na kujenga uwelewa wa masuala ya kiuchumi kijamii pamoja na masuala mtambuka katika kuleta chachu na kuwainua kitaaluma katika kuwainua Viongozi vijana hatimae kuwa tayari na wajibikaji
Ameuomba uongozi wa Raha Tv Online kutoishia bali mafunzo hayo yawe ni endelevu na kuwataka viongozi vijana kuwa wana jukumu kubwa na kuonesha mabadiliko katika jamii na kuonesha uzalendo wenu kwa vitendo kubadilisha akili za baadhi ya watu kwa kutambua Zanzibar ni moja kuikomboa kiuchumi ilipo na kuipeleka kwenye maendeleo zaidi ambayo Serikali yetu inakwendanayo
Amesema Raha Tv Online iwe ni chemchem ya kuwajengea uwezo vijana ili waondokane na utegemezi wawe wabunifu katika utayarishaji kwa uwezo waliokuwa nao kuendeleza vipaji vyao katika kuyasarifu mazingira tuliyonayo na fursa zilizopo.
Mada kadhaa ziliwasiliwa zikiwemo Uzalendo iliyowasilishwa na Bw Mwalimu Ali Mwalimu Katibu Mkuu Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kujitambua na uongozi, Itifaki ndg Mussa Yussuf, uongozi na matumizi ya vyombo vya habari Dkt Mnemo mhadhir chuo cha Habari.
Mada nyengine zilihisu udhalilishaji na maadili Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Taifa ndg Yunus Ali Juma, UKIMWI Mkurugenzi Tume ya UKIMWI Dkt Ahmeid M. Khatib, ushuhuda na historia ya maisha Dkt Rukaiya Wakif Kamishna Idara ya Mipango Zanzibar, mafunzo hayo ya siku mbili yamefanyika kwenye ukumbi wa chuo cha Zanzibar School of Health kilichopo Kwa Mchina mwanzo.